Thursday, December 17, 2009

 

Haki za Wanyama


Hata wanyama wana haki zao na zinastahili kuheshimiwa. Basi hili la abiria jijini Dar es salaam (daladala) ambalo hutoa huduma kati ya Gongo la Mboto na Mwenge limebeba mbuzi ambaye amefungwa juu kana kwamba ni mzigo. Hata nyama inaweza kuwa tamu kweli!

Tuesday, December 08, 2009

 

JK akijibu tu, mipasho itakuwa ruksa





Pichani Rais Kikwete akifafanua jambo wakati akiongea na waandishi wa habari mara baada ya kuwasili jijini Dar es salaam akitokea ziara ndefu iliyohusisha bara la Amerika Kaskazini na visiwa vya Carribea. Kushoto na makamu wa rais, Dk Shein


Rais Jakaya Kikwete jana alirejea nchini akitokea kwenye ziara ndefu iliyomchukua kwenye nchi kadhaa duniani. Alianzia Jamaica akashuka Trinidad na Tobago kabla ya kwenda Cuba ambako alielezea jinsi alivyomuhusudu Che Guevera na baadaye kusogea Marekani kwa uchunguzi wa afya.
Lakini shangwe za mapokezi ziliambatana na maswali juu ya yale aliyoyaacha yakijiri hapa nchini, na hasa ule mdahalo ulioandaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere ambao ulibua maswali mengi juu ya utendaji wa mkuu huyu wa nchi.
Si kawaida kwa watu, hasa wanaotoka kwenye chama kimoja kuhoji utendaji wa kiongozi wao, lakini mawaziri wa zamani, Matheo Qares, Mussa Nkangaa na katibu mkuu wa CCM wa zamani, Phillip Mangula walieleza hofu yao juu ya utendaji wa rais na mwenyekiti wao wa chama. Na Qares alidiriki kusema kama mheshimiwa hataweza kuchukua maamuzi magumu kabla ya 2010, basi CCM haina budi kutafuta mgombea mwingine wa kiti hicho.
Nkangaa, ambaye pia aliwahi kuwa mbunge mkoani Singida, alieleza kuwa chama kimepoteza hadhi yake na sasa kimesahau wafanyakazi na wakulima na kukumbatia matajiri. Mangula alishangazwa na jinsi chama kinavyoendeshwa kwa sasa.
JK alikumbana na maswali kuhusu masuala hayo yote na kwanza akadokeza kuwa hashangazwi na hao waliosema hayo, lakini pili akatoa neno ambalo limenitia shaka kidogo kwamba atakaa na wenzake - bila ya shaka akina Nkangaa, Qares, Mangula, Salim na Warioba si wenzakew- na kujiandaa kujibu hayo makombora.
Ndipo hapo napojiuliza kama kuna umuhimu kwa JK kujibu maoni ya hao waliokosoa utendaji au kufanya kazi nzuri ili iwe majibu tosha kwa wote wenye mashaka naye.
Nadhani JK akithubutu na kuanza kujibu hayo, atakuwa amefungua jukwaa kubwa la mipasho ambalo halitakuwa na msimamizi maana hata rais na mwenyekiti wa chama tawala atakuwa amejitumbukiza katika kushambuliana.
Ndio maana nasubiri kwamba akijibu tu, basi mipasho itakuwa ruksa

 



Jamaa akiimba kile kibao maarufu cha Greatest Love of All huku akisindikizwa na jamaa kibao - labda wengine wako mtungi wakati wa sherehe ya End of the Year za MCL.

 

Ahly, Zamalek ni kufa na kupona leo





Na Mwandishi Wetu
MACHO ya mashabiki wa soka ambao daima huvutiwa zaidi na upinzani wa klabu zinazotoka mji mmoja, leo yataelekezwa Cairo nchini Misri ambako Al Ahly itakuwa ikipambana na Zamalek katika mechi ya daby ambayo inachukuliwa kuwa ina vurugu kubwa kuliko nyingine zote duniani.
Mechi hiyo baina ya timu za jijini Cairo itakuwa ya pili baina ya vigogo hao msimu huu baada ya kushindwa kufungana katika mechi ya kwanza iliyochezeshwa na mwamuzi kutoka Ubelgiji, Frank de Bleeckere.

Mbelgiji huyo atapuliza filimbi tena leo wakati Al Ahly, klabu yenye mafanikio kuliko zote barani Afrika, itakapovaana na wapinzani wao wakubwa wa jijini Cairo.

Kwa sasa Ahly inaongoza msimamo wa ligi kwa tofautin ya pointi tano, ikifuatiwa na Ismailia na ndiyo inayopewa nafasi zaidi ya kuibuka kidedea dhidi ya Zamalek, ambayo imepoteza mechi tatu zilizopita na ambayo iko juu kidogo ya timu zilizo hatarini kushuka.
Kocha mpya wa Zamalek, Hossam Hassan ana wasiwasi na wachezaji wake ambao wana majeraha, hasa mshambuliaji hatari Amr Zaki ambaye anauguza nyonga, wakati Hossam Arafat na Sayed Mosaad hawataweza kucheza mechi hiyo. Kuna mashaka na hali ya Alaa Ali ambaye anaughua mafua.
Upinzani baina ya timu hizo mbili umekuwa wa muda mrefu kiasi kwamba umehamia hadi nje ya uwanja, ukisababisha vifo, uvunjaji wa nyumba na wakati fulani ligi nzima kufutwa.
Vurugu za mashabiki zilisababisha serikali ya Misri kupiga marufuku mechi baina ya klabu kutoka jiji moja kutumia uwanja wa klabu moja na hivyo mechi za wababe hao wawili sasa zinachezwa kwenye uwanja mmoja tu wa Cairo International Stadium.
Upinzani wao umefikia kiwango kwamba hata waamuzi wa Misri hawaaminiki na Chama cha Soka cha Misri sasa kinalazimika kutumia marefa kutoka barani Ulaya ili kuondoa upendeleo.
Mwamuzi mkongwe Kenny Clark, ambaye aliwahi kuchezesha mechi nne za Old Firm, yaani baina ya vigogo wa Glasgow nchini Scotland, Celtic na Rangers, aliteuliwa kuchezesha mechi ya watani hao mwaka 2001 baada ya vyama sita vya soka barani Ulaya kukataa kutuma waamuzi wake.
Kabla ya hapo, mechi iliyochezeshwa na mwamuzi wa Ufaransa Mark Batta, ilivunjika baada ya wachezaji wa Zamalek kugoma kuendelea na mchezo wakipinga mchezaji wao, Ayman Abdel Aziz kuonyeshwa kadi nyekundu katika dakika yab pili kwa kukwatua kwa nyuma.
Asili ya upinzani baina ya timu hizo unasemekana kuanzia nyakati ambazo majeshi ya Uingereza yalikuwa kwenye mitaa ya jiji la Cairo. Wakati huo, mpira wa miguu ulikuwa ukichukuliwa kama utamaduni pekee uliojipenyeza kwenye nchi ya Misri, lakini iliichukua nchi hiyo miaka kadhaa hadi 1907 ilipoanzisha klabu ya kwanza ya soka, Al Ahly, iliyokuwa ikiendeshwa na wenyeji.
Ikapewa jina la Al Ahly kumaanisha Taifa na rangi zake zikawa nyekundu ya zamani ambayo ilikuwa ikitumika kabla ya wakoloni wa Kiingereza kuvamia nchi hiyo. Al Ahly ikawa ikichukuliwa kama klabu kwa ajili ya taifa hilo, ikikutanisha watu wa kada mbalimbali na matabaka mbalimbali.
Zamalek, ambayo huvalia rangi nyeupe, ilikuwa ikichukuliwa kama klkabu ya nje na ya watui wa nje. Pia ilikuwa klabu ya mfalme ambaye alikuwa akichukiwa, King Farouk. Awali klabu hiyo ilipewa jina la mfalme huyo, lakini ikabadilishwa na kuitwa Zamalek baada ya mfalme huyo kuondolewa.
Mwanzoni timu hiyo ilikuwa na mashabiki ambao ni Waingereza na watu wa nje ambao hawakupenda mwenendo mpya wa utaifa wa Misri. Kwa hiyo upande mmoja ukawa wa rangi nyekundu yab watu maskini na wanaojivunia utaifa wao wakati upande mwingine ukawa wa matajiri, wa daraja la kati na wanaotaka mabadiliko.
Makundi hayo yapo hadi leo.
Klabu hizo mbili si bora nchini Misri tu, bali Afrika nzima huku Al Ahly ikiwa imetangazwa kuwa klabu bora ya karne na Shirikisho la Soka Afrika (CAF).

 

Mangula auchambua
uongozi wa Kikwete

Sadick Mtulya
UTAWALA wa Rais Jakaya Kikwete umezidi kukosolewa baada ya katibu mkuu wa zamani wa CCM, Philip Mangula kuuchambua, akisema unasumbuliwa na mambo matatu makubwa, ikiwa ni pamoja na kupeana uongozi kwa urafiki.
Mangula anaendeleza mjadala wa siku za karibuni ambao umekuwa shubiri kwa CCM, ambayo imelazimika kutoa kauli kadhaa kujibu mashambulizi dhidi ya mwenyekiti wake.
Makada wa mwisho kuikosoa serikali ya Kikwete walikuwa mawaziri wa zamani, Matheo Qares na Juma Nkangaa ambao walieleza wasiwasi wao kama mkuu huyo wa nchi ana uwezo wa kufanya maamuzi magumu na kwamba CCM imepoteza mwelekeo kwa kuamua kukumbatia wafanyabiashara na kuachana na sera yake ya kuwa chama cha wakulima na wafanyakazi.

Safari hii, Mangula ambaye alikuwa mtendaji Mkuu wa CCM kabla ya kuteuliwa kwa Makamba, ameibuka na kueleza udhaifu wa chama hicho tawala na kikongwe barani Afrika na ambacho hakuna shaka kwamba kinapitia kwenye wakati mgumu kwa sasa.

Mangula ambaye alihudhuria kongamano la Mwalimu Nyerere jijini Dares Salaam ambalo liliibua hoja nyingi dhidi yab serikali ya Kikwete wiki iliyopita, hakuchangia maonin yake katikam mjadala huo, lakini
baadaye alifanya mahojiano na Mwananchi na kutaka mambo matatu ambayo yanautafuna uongozi wa Rais Kikwete.

Mangula alitaja mambo hayo kuwa ni ubinafsi, kufanya maamuzi kabla ya kuelimisha wananchi na kuwepo kwa wigo finyu wa majadiliano na wadau katika masuala mbalimbali.

Mangula, ambaye alishika nafasi ya katibu mkuu wa CCM kwa kipindi cha miaka kumi ya uongozi wa serikali ya awamu ya tatu, alitahadharisha kuwa iwapo mambo hayo hayatarekebishwa kwa haraka na kwa kipaumbele kinachostahili, taifa litaelekea pabaya zaidi.

“Utawala wa sasa umetofautiana na tawala nyingine kwa kupungukiwa na mambo matatu ya msingi ambayo ni ubinafsi, kufanyika maamuzi kabla ya kuelimisha wananchi pamoja na kutokuwepo kwa wigo mpana wa majadiliano kuhusu masuala mbalimbali ya mustakabali wa taifa,” alisema| Mangula.

Mangula alisema hali hiyo imesababishwa na watu wengi wanaopewa uongozi kutokuwa sifa za kuongoza na kwamba wamepata nafasi hizo kwa njia za urafiki.

“Hata utaratibu mzima wa kuwapata viongozi wanaostahili kwa sifa haupo, badala yake mambo yanafanywa kwa urafiki,” alisema Mangula ambaye amekuwa kimya kwa muda mrefu.

Akifafanua hoja zake hizo, Mangula alisema katika utawala wa sasa ubinafsi ndio umeonekana kuchukua kipaumbele katika kutatua mambo muhimu ya kitaifa.

Mangula aliweka bayana kwamba katika utawala uliopita ubinafsi haukupewa nafasi kwa kuwa kabla kiongozi hajazungumzia jambo lolote, alilazimika kupata mawazo ya chama tawala na wanachama kuhusu anachotaka kuzungumza.

Aliongeza kwamba kutotumika kwa mfumo huo ndio sababu ya kupishana kwa kauli za viongozi kunakoendelea kutamba kwenye safu za mbele za vyombo vya habari kwa sasa.

“Tabia ya kutaka kuonekana kuwa wewe ni bora kuliko mwingine ipo, ndio maana leo viongozi, tena wa kutoka chama kimoja, wanapishana kauli kuhusu jambo moja,” alifafanua.

Akizungumzia kufanyika kwa maamuzi kabla ya kuwaelimisha wananchi, Mangula alisema hilo ni tatizo linaloendelea kulalamikiwa na Watanzania.

Mangula alisema katika utawala uliopita watu walielimishwa kwanza kabla ya kufikiwa kwa maamuzi.
“Utaratibu wa kuelimisha kwanza kabla ya kufikiwa kwa maamuzi ndio uliokuwa ukitumika, lakini hali sasa inaonekana kuwa tofauti,” aliongeza.

Kuhusu kutokuwepo kwa wigo mpana wa majadiliano katika masuala ya kitaifa, Mangula alisema hiyo inatokana na viongozi wachache waliopewa dhamana na wananchi kuamini kuwa mawazo yao yanajitosheleza.

Hoja za Mangula, ambaye kwa sasa anajishughulisha na masuala ya kilimo, zinashabihiana na zile zilizowahi kutolewa na mawaziri wakuu wawili wastaafu, Dk Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Warioba kuhusu mustakabali wa taifa.

Jaji Warioba alinukuliwa na vyombo vya habari hivi karibuni akitahadharisha kuwa nchi inaelekea kubaya kutokana na mambo mbalimbali kuendeshwa kinyume.

Warioba, ambaye alishika nafasi hiyo ya mtendaji mkuu wa serikali kwenye miaka ya themanini, alifafanua kuwa taifa linakabiliwa na matatizo mengi ikiwemo ukosefu wa maadili ya uongozi, rushwa na hata utaratibu mzima wa kuendesha mambo na kubainisha kuwa kuna pengo kubwa katika kuaminika kwa serikali.

Naye Dk Salim Hamed Salim, ambaye aliwahi kuwa katibu mkuu wa Umoja wa Afrika (OAU), alisema mfumo wa serikali ya Tanzania kwa sasa umeoza kwa rushwa na hivyo hauwezi kumsaidia rais kuikabili, hivyo rushwa kutawala kuliko kitu kingine.

Dk Salim alisema wakati wa utawala wa awamu ya kwanza wa Mwalimu Julius Nyerere, rushwa ilidhibitiwa kikamilifu, lakini wakati huu rushwa imeachiwa nafasi kubwa na kufanya hali ya Watanzania idorore.

Alisema tofauti kubwa kati ya awamu hizo na ile ya Mwalimu Nyerere ni kuwa muasisi huyo wa taifa alionyesha kwa vitendo kuwa rushwa ni jambo aliloamua kulifungia mkanda na kupambana nalo, lakini baada ya hapo tatizo hilo limeachiwa liendelee kiasi cha rushwa kugeuka kuwa utaratibu.

Mwanadiplomasia huyo aliongeza kwamba, licha ya nia njema ya Rais Kikwete ya kupambana na rushwa na ufisadi, bado mfumo mzima wa serikali umeoza kiasi ambacho haiwezekani kupambana na rushwa.

Baadaye wakati wa kongamano lililoandaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere, Qares, ambaye alikuwa Waziri wa Menejimenti ya UItumishi wa Umma katika serikali ya awamu ya tatu, na Nkangaa ambaye alikuwa waziri katika serikali ya awamub ya pili, waliibuka.

Qares alimtaka Rais Kikwete awe jasiri na kufanya maamuzi magumu na akashauri kuwa akishindwa kufanya hivyo hadi 2010, CCM isimpitishe kugombea urais 2010.

Qares, ambaye pia aliwahi kuwa mkuu wa mkoa wakati wa uongozi wa Benjamin Mkapa, alisema Rais anapaswa kufumba macho na kuwashughulikia hata wale wanaosema hakukutana nao barabarani.

Naye Nkangaa alisema CCM imepoteza heshima yake na kubaki kuwa chama cha matajiri wachache na kutupa mkono wakulima na wafanyakazi, ndiyo maana inasuasua kuwachukulia hatua watuhumiwa katika kashfa za Kagoda na Richmond.

Tangu kutolewa kwa ripoti ya kashfa ya utoaji zabuni ya uzalishaji umeme wa dharura kwa kampuni ya Richmond, wabunge wa CCM wamekuwa wakitofautiana sana katika hoja, baadhi wakiunga mkono kujiuzulu kwa Edward Lowassa katika nafasi ya uwaziri mkuu na kutaka hatuia zaidi zichukuliwe, huku wengine wakipinga.
Hali ilizidi kuwa mbaya katika mkutano uliopita wakati wabunge walipoicharukia serikali yao wakiituhumu kufanya mambo kwa ubinafsi na kubariki mikataba mibovu, na mjadala huo uliilazimisha CCM kuitisha mkutano wake wa Halmashauri Kuu.
Lakini mkutano huo ukawa moto mbaya zaidi baada ya Spika Samuel Sitta kunusurika kuvuliwa uanachama kutokana na kundi linalotuhumiwa kwa ufisadi kujipanga vyema kushughulikia wanaowatuhumu.
Mijadala mikali kwenye kikao cha Halmashauri Kuu iliisha kwa CCM kuunda kamati ya wazee wa busara, ikilongozwa na rais wa serikalinyab awamu ya tatu, Ali Hassan Mwinyi ambayo mwezi uliopita ilisababisha kizaazaa kingine wakati ilipoongea na wabunge kuhusu kudhoofika kwa mahusiano baina ya wanachama na viongozi wa chama hicho tawala.
Lakini mkutano huo ukawa jukwaa zuri kwa watuhumiwa wa ufisadi kujibu mashambulizi yanayotolewa kila mara hadharani dhidi yao na hasa kwenye vikao vya Bunge.
Katika mikutano hiyo ya Kamati ya Mwinyi, makamanda wa vita dhidi ya ufisadi walijikuta wakibebeshwa tuhuma nzito na kutolewa maneno machafu, kiasi kwamba hali ndani ya CCM ikaonekana kuwa si shwari na haikuwa ajabu wakati mawaziri hao wa zamani pamoja na Mangula kujitokeza na kuuchambua utawala wa Kikwete kuwa una matatizo.

This page is powered by Blogger. Isn't yours?