Friday, April 28, 2006

 

Nani aingie kudhamini klabu zisizo na uhakika

MIAKA minne iliyopita nilitumwa Arusha kwenda kuandika habari ya mechi ya Ligi Kuu ya Vodacom kati ya Yanga na Arusha FC.
Kama kawaida niliondoka asubuhi Dar es Salaam na kufika Arusha majira ya saa 11.00 jioni na kwa kuwa lazima wageni wapewe nafasi ya kutumia uwanja siku moja kabla ya mechi, nilipitiliza kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid kuangalia mazoezi ya Yanga.
Lakini cha kushangaza nilikuta vijana wa Rolling Stones wakiendelea na mazoezi.
Nilikuwa mmoja wa umati wa watu walioshikwa na butwaa kutoiona Yanga na ambao moja kwa moja waliingiwa na wasiwasi kuwa mechi hiyo ambayo ingefanyika Jumamosi, yaani kesho yake.
Nilipomuuliza mmoja wa viongozi wa soka wa Arusha kuhusu kutofika kwa Yanga, yeye ndiye aliyenishangaa kwamba eti sina taarifa kuwa mechi hiyo imearishwa hadi wikiendi iliyokuwa inafuata.
Gharama ambazo kampuni yangu ya wakati huo iliingia kwa ajili ya kupata taaifa za mechi hiyo, zilikuwa zimekwenda bure na nililazimika kuanza kuandaa safari ya kurudi Dar kuendelea na shughuli nyingine.
Hayo ndiyo matatizo yanayokumba wadau wengi wa soka - mambo kuendeshwa bila ya kutabirika na hivyo kutokuwepo kwa mipango itakayowezesha wadau kuhusika kwa njia moja au nyingine katika mechi za soka.
Mechi ya soka haihusu timu mbili zinazokutana peke yake, bali wadau wengine wote wanaozunguka mchezo huo - yaani wafanyabiashara wadogo kwa wakubwa, vyombo vya habari, wadhamini na watu wengine wote wanaoweza kutumia soka kuendesha maisha (lakini si kwa ujanja ujanja).
Kwamba unapokuwa umepanga mechi itafanyika Desemba 20 mwaka huu na usiibadili tarehe, maana yake vyombo vya habari vitaweza kujipanga jinsi ya kuishughulikia mechi hiyo - kwa njia moja kupata wateja wengi zaidi na kwa njia nyingine kuhamasisha umma.
TV zitaweza kufikiria kama zitaweza kununua haki za kutangaza mechi hiyo, wakati bendi zitafikiria jinsi ya kujinufaisha kwa kwenda kufanya onyesho mkoani humo jioni ya siku ya mechi. mahoteli yatafikiria jinsi ya kupata wateja watakaoenda kuangalia mechi hiyo na wadhamini watafikiria jinsi ya kudhamini timu hizo ili wajitangaze kibiashara.
Kuna mambo mengi yanayoonyesha kuwa mechi moja ya soka inahusu mambo mengi kwa maana hiyo kuwa na uhakika wa kueleweka kuwa mechi itafanyika siku fulani kunatoa mwanya kwa wadau kujipanga vizuri.
Leo hii ushiriki wa Yanga na Simba kwenye michuano ya Kombe la Kagame hauko bayana, hivi nani anaweza kuanza kujipanga kibiashara, kikazi au kijamii kwa ajili ya mashindano hayo?
Hivi mdhamini gani ataweza kuingia na kuweka fedha zake kuidhamini Yanga au Simba kwenye michuano hiyo wakati hadi sasa klabu hizo bado zinatoa kauli zisizoeleweka kuhusu ushiriki wao kwenye Kagame?
Kama Yanga hadi jana imesema haitashiriki michuano hiyo, itawezaje kupata wadhamini katika hali kama hiyo.
Klabu zetu lazima zijifunze kuwa wakati ule wa kujiendesha kiholela umekwisha.
Viongozi wa klabu hizo hivi sasa walitakiwa wawe wanazunguka kwenye makampuni kujaribu kuyashiwishi jinsi yatakavyonufaika na mashindano ya Kagame iwapo yatadhamini klabu hizo kutokana na ushindani ulio katika mashindano hayo na jinsi zilivyo na mvuto.
Hiyo asilimia 25 ya mapato ambayo klabu hizo zinadai zitakuwa kubwa kiasi gani kama hata mashabiki hawana uhakika wa ushiriki wa timu hizo katika michuano ya Kombe la Kagame?
Kwa karibu misimu mitatu sasa, Yanga inashiriki Ligi Kuu bila ya mdhamini wa kueleweka na hii itaweza kuendelea kama uongozi hautakuwa imara katika mambo yake na kuwa unatoa kauli zinazochanganya hata hao wanaofikiria kuidhamini.
Klabu hizi mbili hazina budi kuanza sasa kuwa na mipango ya muda mrefu na iliyo imara ili ziweze kushawishi wadhamini kutumbukiza fedha zao kwenye klabu hizo, lakini pia kuwafanya mashabiki waweze kujipanga vizuri kwa ajili ya mechi zao ili zinufaike kwa mapato.
Wasipobadilika wataendelea kugombea mapato ya milangoni, ambayo kwa klabu kubwa ni sehemu ndogo sana ya mapato ya kuendeshea klabu.

Thursday, April 27, 2006

 

Waziri Bendera, mengi yanakusubiri michezoni

KWA mapitio ya haraka haraka tu ni kwamba karibu kila mpenda michezo amefurahishwa na uteuzi wa kocha wa zamani wa timu ya taifa ya soka, Taifa Stars, Joel Bendera kuwa naibu waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, ambaye anajikita zaidi kwenye michezo.
Naweza kuhisi kuwa kukubalika kwa uteuzi huo kunatokana na ukweli kwamba Bendera, ambaye pia alikuwa mwenyekiti wa Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kabla ya kuvuliwa siku moja kabla ya uchaguzi mkuu Desemba 14 kutokana na kumaliza muda wake, ni mwanamichezo halisi ambaye ameshiriki kwa kiasi kikubwa kujaribu kuinua michezo na hasa soka.
Kwa maana hiyo, kupewa dhamana ya kuongoza michezo ni uteuzi mwafaka na ambao umekuja kwa wakati muafaka.
Kwanza ana shahada ya pili ya elimu ya viungo, akiwa amejikita zaidi katika ualimu wa soka, ana diploma ya ualimu wa soka, amepitia kozi mbalimbali za uongozi wa michezo na ameshakuwa mwalimu wa soka, na cha zaidi ameshakuwa mwaliku wa Chuo cha Elimu Korogwe.
Hayo peke yake yanaonyesha ni kiasi gani, wizara hiyo imempata mwenyewe.
Lakini Bendera, ambaye atakuwa chini ya Waziri Mohamed Seif Khatib, anaingia madarakani wakati kukiwa na mabadiliko mengi na hasa kwenye katiba za vyama vya michezo na klabu zikiwa zimefanyiwa marekebisho makubwa.
Tena mabadiliko hayo ni yale yanayoiondoa serikali katika shughuli za vyama hivyo na klabu, na kama Mheshimiwa Bendera atakumbuka mgogoro wa mwisho aliopambana nao ni huu wa Chama cha Riadha Tanzania (TAAA), ambacho sasa kimejibadilisha jina na kuwa AT.
Kuondolewa kwa serikali kwenye katiba za vyama hivyo kunalifanya Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kuonekana linaondokewa na majukumu ambayo iliyazoea.
Sasa BMT haina mamlaka yoyote juu ya vyama vingi vya michezo, likiwemo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) na Shirikisho la Mpira wa Kikapu (TBF), lakini sheria ya nchi bado linaitambua BMT kama chombo cha serikali chenye maamuzi ya juu katika michezo kabla ya waziri husika.
Ni kwa maana hiyo ndiyo nafikiri kuwa Mheshimiwa Bendera atakuwa na kazi ngumu ya kutafsiri upya majukumu ya BMT katika usimamiaji michezo baada ya mabadiliko hayo ya vyama na hasa katika kipindi hiki, ambacho Mheshimiwa Rais, Jakaya Kikwete ameahidi kusaidia vyama katika sekta ya ufundi.
BMT itakuwa na nafasi gani ya kuhakikisha msaada huo wa serikali unatumika ipasavyo kama vyama havilitambui tena baraza hilo.
Lakini Bendera pia ameingia wakati ambapo serikali imeahidi kurudisha michezo mashuleni. Hapa Bendera na waziri wake watakuwa na kazi ngumu ya kutengeneza tena mkakati wa kuhakikisha michezo inafundishwa vipi mashuleni kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu.
Tunajua pia kuwa serikali haitakiwi kulazimisha michezo kuendeshwa kwa malipo (professional) bali vyama husika kama soka, ngumi na kikapu, lakini inaweza kujenga mazingira yatakayowezesha michezo kuwa ajira ya uhakika.
Na hili litawezekana kama Wizara ya Habari, Utamaduni na Michezo itakaa pamoja na wenzao wa Wizara ya Kazi kufikiria kuweka mazingira ambayo yataifanya hiyo ajira, ambayo inasemekana imeshajengwa kwenye michezo kama soka na ngumi, kuwa ya uhakika.
Kuandikiana mikataba ya kulipana fedha kana kwamba za kusaidia, hakufanyi soka kuwa ya kulipwa. Ukweli kwamba wanasoka wanategemea mchezo huo kuendesha maisha yao hakufanyi soka ikawa ya kulipwa.
Kuna mambo muhimu ambayo yanatakiwa yaangaliwe na wizara hizo mbili na pengine hata ile ya fedha kuhakikisha kuwa soka na michezo mingine yenye uwezo wa kuvuta mashabiki wengi, wadhamini na kuingiza fedha, inatengeneza ajira zenye uhakika na za kudumu.
Pia vyama kwa sasa vina mikakati yake ya muda mrefu ya maendeleo, ambayo kwa kiasi fulani yatakuwa na manufaa kwa taifa kiuchumi, kijamii na kisiasa kwa maana hiyo serikali lazima iweke mkono wake kuhakikisha malengo hayo yanafanyika.
Huu ni wakati wa kuangalia serikali itajihusishaje licha ya kwamba vyama hivyo vimeiondoa serikali katika shughuli zake.
Yapo mengi sana ambayo Mheshimiwa Bendera na bosi wako mtatakiwa myaangalie kwa makini wakati mtakaposhika ofisi zenu kuanzia Jumatatu.
Sisi wapenzi wa michezo tumekaa kusubiri kuona kasi mpya, ari mpya na nguvu mpya inatafsiriwa vipi katika utendaji.

This page is powered by Blogger. Isn't yours?